Thursday, May 29, 2014

Baada Ya LHRC Kuzindua Ripoti Ya Taarifa Kuhusu Madhara Yanayotokana Na Uchimbaji Baadhi Ya Wananchi Waeleza Haina Haja Serikali Kusitisha Uchimbaji

Siku moja baada ya kituo cha sheria na haki za binaadamu LHRC,  kuzindua  ripoti ya taarifa kuhusu madhara kwa afya na mazingira ya madini ya urani,  baadhi ya wananchi wamesema  hakuna haja ya Serikali kusitisha uchimbaji wa madini hayo, badala yake ziwekwe njia madhubuti za kudhibiti madhara.  
Wakazi hao VEDASTO MKAKA, MAIMUNA IDDY, NA ADNANI MITEMA wamesema,  uzoefu unaonyesha kuwa sio Tanzania  pekee yenye madini kama hayo, hivyo kuacha kuyachimba kwa kuhofia madhara sio jambo la msingi, na wametumia fursa hiyo kuwaomba wanaharakati hao kushirikiana na serikali, kutafuta ufumbuzi wa hali hiyo. 
 
Aidha akizungumza katika uzinduzi huo, mkurugenzi wa  kituo cha sheria na haki za binaadam  Bi. HELEN KIJO BISIMBA amesema, uzoefu  wa kitaalamu kutoka katika nchi ambazo madini hayo yanazalishwa unaonesha kuwa, zoezi la uchimbaji wa madini hayo linahitaji  kiwango kikubwa cha maji, huku athari kwa jamii  kuhusu magonjwa ya ngozi na kansa ikihofiwa kuwa kwa kiasi kikubwa.
Naye makamu mwenyekiti wa tume ya haki za binadamu na utawala bora  MAHAFUDHA HAMID amesema,  uzoefu kutoka katika machimbo mengi ya madini hapa nchini unaonesha kuwepo kwa baadhi ya vitendo vya uvunjifu wa haki za binaadamu hivyo vyema sera ya madini ya urani ikawekwa wazi kutokana  na hatari iliyomo katika madini hayo, ili kuepusha vitendo hivyo kutojitokeza.
Nayo baadhi ya Maeneo yaliyofanyiwa utafiti na kubainika kuwa na madini ya urani ni  Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.
Miongoni mwa maeneo hapa nchini ambayo madini ya urani yanategemewa kupatikana ni pamoja na NAMTUMBO, MANYONI na BAHI.

No comments:

Post a Comment