Thursday, May 29, 2014

Watendaji Wa Halmashauri Ya Wilaya Ya Mbulu Wameagizwa Kuhakikisha Wanaweka Mipango Mizuri Ya Matumizi Bora Ya Ardhi

Watendaji wa Halmashauri ya wilaya ya MBULU mkoani MANYARA wameagizwa kuhakikisha wanaweka mipango mizuri ya matumizi bora ya Ardhi, ili kuepusha migogoro baina ya WAFUGAJI na WAKULIMA inayosababisha wakati mwingine umwagikaji wa Damu.
Katibu mkuu wa Chama cha Mapinduzi CCM, ABDULRAHMAN KINANA ametoa kauli hiyo, baada ya kutembelea eneo la bonde la YAEDA wilayani humo, na kupata malalamiko ya wananchi hao kuhusiana na mgogoro wa Ardhi kati ya WAFUGAJI, WAKULIMA na WAWEKEZAJI, wanaodaiwa kudhulumu ardhi ya wanyonge katika eneo hilo.
Wakitoa malalamiko hayo kwa katibu mkuu  wa CCM,  wananchi hao wamedai kuwepo kwa kikundi cha watu kinachotumia mabavu na fedha,   kuwaondoa  kutoka katika maeneo yao ya Asili kwa lengo la kutwaa ardhi ya wananchi hao ambao wengi wao ni masikini.
Kufuatia malalamiko hayo katibu mkuu wa CCM amekiri kuwa, migogoro mingi ya Ardhi inayochukua sura mpya kila siku na umwagikaji wa damu kwa wasiokuwa na hatia, inachangiwa zaidi na Watendaji wa Serikali kushindwa kutoa elimu kuhusu matumizi bora ya Ardhi kwa Jamii za WAFUGAJI na WAKULIMA, huku mkuu wa wilaya ya Mbulu ANATOLY CHOYA akielezea mikakati ya Serikali katika kukabiliana na tatizo hilo. 
Mkoa wa MANYARA ni miongoni mwa maeneo yenye migogoro mingi ya Ardhi, inayochangia umasikini kwa watu wake kwa kuwa wanatumia muda mwingi katika kushughulikia migogoro hiyo, kuliko kufanya kazi za Maendeleo.

No comments:

Post a Comment